skip to Main Content
P.O. Box 65001, MUHAS,Dar es Salaam webmaster@muhas.ac.tz 0752360543 / 0756265177 - Admission Office
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Juma Selemani Mkomi akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo ya Stadi za Uongozi na Menejimenti kwa viongozi wa MUHAS
 Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi, Prof. Andrea Pembe akitoa salamu za ukaribisho wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Stadi za Uongozi na Menejimenti kwa viongozi wa MUHAS
 Kaimu Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt Ernest Francis Mabonesho akimkaribisha Mgeni Rasmi kufungua Mafunzo ya Stadi za Uongozi na Menejimenti kwa viongozi wa MUHAS
 Washiriki wa mafunzo  Stadi za Uongozi na Menejimenti wakifuatilia  hotuba mbalimbali wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo 
Washiriki wa mafunzo pamoja na wawezeshaji wakiwa katika picha ya pamoja na Mgeni Rasmi  mara baada ya kufungua Mafunzo ya Stadi za Uongozi na Menejimenti, MUHAS

KATIBU MKUU UTUMISHI AFUNGUA MAFUNZO YA UONGOZI MUHAS

30 Mei, 2023

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Juma Selemani Mkomi leo amefungua rasmi Mafunzo ya Stadi za Uongozi na Menejimenti kwa viongozi wa ndaki, Shule kuu, kurugenzi, vitengo na idara mbalimbali za Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili, MUHAS.

Akizungumza katika ufunguzi huo, Katibu Mkuu, Bw. Juma Mkomi ameupongeza uongozi wa MUHAS kwa kuona umuhimu wa kutenga fedha na kugharamia mafunzo haya ambayo ni muhimu sana kwa viongozi waandamizi wa umma ili kuboresha utendaji serikalini.

Kwa kufanya hivi, Katibu Mkuu amesema uongozi wa MUHAS unakuwa umeitikia wito wa Serikali kwa kupitia Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakutenga fedha kuwapeleka watumishi kuhudhuria mafunzo.

“Nina imani kwamba mafunzo haya mnayoyapata yataenda kuongeza ufanisi katika maeneo yenu ya kutolea huduma mbalimbali”, Bw. Mkomi aliongeza.

Akitoa salamu za ukaribisho, Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Andrea Pembe alieleza kuwa lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo viongozi wa MUHAS kwenye nafasi zao mbalimbali ili kuboresha utendaji wao na kutoa huduma bora inayotarajiwa.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi kufungua mafunzo haya, Kaimu Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt Ernest Francis Mabonesho, alieleza kuwa pamoja na mada zingine washiriki wa mafunzo haya watajifunza masuala ya itifaki na ustaarabu, sheria ya utumishi wa umma, uendeshaji wa mashauri ya nidhamu, uongozi wa kimkakati, utaratibu wa kufanya maamuzi, utunzaji wa kumbukumbu za serikali katika utumishi wa umma na usalama wa taarifa za serikali.

Mafunzo hayo ya siku tatu yanatolewa na wawezeshaji kutoka Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, TPSC na kufanyika kwenye ukumbi wa mikutano, MUHAS, jengo la CHPE.