









06 Aprili 2022
Katibu Mkuu, Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi amewapongeza Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili kwa kuwa mstari wa mbele katika kuibua changamaoto za sekta za afya.
Prof Makubi ameyasema hayo leo wakati wa akifungua Kongamano la Nane la Kusambaza Matokeo ya Utafiti la Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili lililojikita katika Saratani ya Damu
Akizungumza katika Kongamano hilo, Katibu Mkuu huyo amesema MUHAS ni moja ya taasisi ambazo ziko mstari wa mbele kwenye magonjwa mbali mbali, japokuwa haijasikika ikiongelea kuhusu saratani za damu. Prof. Makubi amewapomgeza kwa kuamua kuvunja ukimya huu kwa kupanga kusanyiko hili la wasomi, watafiti, wanafunzi, wawakilishaji wa wagonjwa, na watanzania wenzangu kwa ajili ya kuelimishana kuhusu saratani za damu na kubadilishana mawazo ya namna bora ya kutoa huduma kwa wagonjwa wenye saratani za damu.
Akielezea Takwimu za Saratani ya Damu, Prof. Makubi amesema takwimu za Shirika la Afya Duniani kupitia Shirika la Kimataifa la Utafiti wa Saratani zinaonyesha kuwa, takribani watu elfu arobaini wanagundulika kuwa na saratani kila mwaka hapa Tanzania, na asilimia themanini ya wagonjwa hawa hupoteza maisha ambapo asilimia kumi ya saratani hizi ni saratani za damu.
Kwa kutambua hilo Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, vyuo vikuu na taasisi nyingine, imeendelea kusomesha na kuzalisha wataalam wa afya wa kada mbali mbali, wakiwemo wataalam wa maabara, wauguzi, madaktari, madaktari bingwa na wabobezi wa saratani ya damu. Hii imesaidia sana, kuimarisha huduma za afya katika hospitali za rufaa mbali mbali nchini, kwa wagonjwa wenye saratani za damu.
Prof. Makubi amesema, kama taifa linajivunia kuwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili ambacho ndicho Chuo kinachoongoza Tanzania kuelimisha wataalam mbali mbali wa afya kuanzia ngazi ya shahada ya kwanza mpaka ngazi ya juu ya madaktari bingwa wabobezi na wataalam wa vitengo mbali mbali vikiwemo vya maabara.
Katibu Mkuu aliongeza kwamba MUHAS wamekuwa mstari wa mbele katika kuibua changamoto za sekta ya afya na kutoa shauri mbalimbali ambazo zinaendelea kuboresha maisha ya mtanzania kupitia tafiti. Amesema kuwa tafiti ni chachu ya maboresho na maendeleo ya huduma za afya.
Akielezea lengo kuu la Kongamano hili Makamu Mkuu wa Chuo Prof. Andrea Pembe amesema ni kukutanisha wadau mbalimbali wa magonjwa ya saratani ya damu nchini ikiwemo watunga sera, watumishi wa sekta ya afya, watafiti, wanataaluma na washiriki wenza wanaosaidia kutekeleza shughuli zinazohusisha saratani ya damu na magonjwa mengine yasiyoambukiza.
“Kama tunavyotambua wanasayansi ni watu muhimu katika jamii wanaofanya tafiti za kujua vyanzo vya matatizo na kutoa ufumbuzi wa matatizo hayo. Kongamano hili ni sehemu muhimu ya kusikia kutoka kwa wanasayansi wetu, sio tu kuhusu changamoto, bali pia mapendekezo yao ya namna ya kutatua changamoto hizi,” Alisema Prof. Pembe
Katika Kongamano hili Katibu Mkuu, Wizara ya Afya aliwapa tuzo kwa Dkt. Pius Magesa, Dkt. Trish Scanlan na Dkt. Khamza Maunda kwa kutambua mchango wao katika fani ya hematolojia na kwenye maswala ya saratani ya damu.