23 Aprili 2021
Wanawake wa MUHAS wamepatiwa mafunzo ya ujasiriamali ili kupata elimu ya kuweza kuanza ujasiriamali kwa ambao hawajaanza na kwa walioanza kukuza biashara zao zaidi.
Mafunzo hayo yametolewa na mtaalamu wa ujasiriamali kutoka Kampuni ya ENSOL Limited, Bw. Prosper Magari, ambapo washiriki walipata elimu kuhusu Maana ya Ujasiriamali, Jinsi ya Kuanza Biashara (Nitaanzaje), Kodi za Biashara na Elimu kuhusu Mikopo. Pia washiriki waliweza kujadili mada zilizotolewa na kuuliza maswali kwa ajili ya ufafanuzi zaidi.
Vile Vile Mkuu wa Kitengo cha Programu ya Jinsia (Gender Program Unit) Dkt. Hawa Mbawala alishukuru uongozi wa MUHAS kwa kuwawezesha kuandaa haya mafunzo kwa ajili ya wanawake wa MUHAS na pia alimshukuru mtoa mada kwa ufafanuzi mzuri wa mada husika ambao utawahamasisha wanawake kubuni shughuli mbalimbali za ujasiriamali ili kuongeza vipato vyao.
“Moja ya mambo ambayo MUHAS inafanya katika kuimarisha ustawi wa wafanyakazi ni kuhakikisha hakuna mtumishi ambaye hajui kesho yake, na haya yanafanyika kwa kuandaa semina kama hizi ili kuwapa ujuzi watumishi wake ambapo watatumia ujuzi huu hata baada ya kustaafu au wakiwa nje ya MUHAS,” Dkt. Hawa alisema.
Mafunzo haya yaliandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi, Muhimbili kupitia Kitengo chake cha Programu ya Jinsia.